Na Fidelis Butahe na Habel Chidawali, Mwananchi
Dar/Dodoma. Wakati Katiba inayopendekezwa ikikabidhiwa kesho kwa Rais Jakaya Kikwete, Mwenyekiti wa iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba amesema hata akialikwa katika sherehe hizo hatahudhuria kutokana na majukumu aliyonayo kwa sasa.

Mwenyekiti wa iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba.PICHA|MAKTABA
Jaji Warioba alisema angependa kuhudhuria sherehe hiyo ambayo pia itahudhuriwa na wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba, wakuu wa mikoa, mabalozi na wageni mbalimbali, lakini kutokana na dharura aliyoipata haitawezekana.
Sherehe hiyo itafanyika mkoani Dodoma kesho na Mwenyekiti wa lililokuwa Bunge Maalumu la Katiba, Samuel Sitta atakabidhi nakala ya Katiba inayopendekezwa kwa Rais Kikwete na Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohammed Shein.
Katika hafla hiyo itakayofanyika kwenye Uwanja wa Jamhuri, wajumbe wa Bunge hilo walioshiriki mchakato huo kuanzia mwanzo mpaka mwisho watapewa vyeti.
Akizungumza na gazeti hili jana, Jaji Warioba alisema hadi jana hakuwa amepata mwaliko lakini hata kama akipewa hataweza kuhudhuria. “Siwezi kutoka nje ya Dar es Salaam kwa siku mbili tatu hizi kwa sababu nina dharura. Kama wakinialika nitawaomba radhi kwamba sitaweza kuhudhuria,” alisema.
Alipoulizwa iwapo Jaji Warioba ni miongoni mwa waalikwa katika sherehe hiyo, Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Dk Rehema Nchimbi alisema angetoa majibu leo kuhusu suala hilo lakini anaamini mkongwe huyo ni miongoni mwa viongozi wastaafu, hivyo kualikwa ni lazima.


